Gavana wa kaunti ya Narok, Patrick Ole Ntutu amewaonya wakaazi wa gatuzi dogo la Transmara Magharibi dhidi ya kushambulia, kuzuia au kutekeleza aina yoyote ya ghasia kwa mtumishi wa umma anayetoa huduma kwa umma kihalali.
Ntutu alisema kuwa yeyote yule atakayepatikana katika makosa ya aina hii basi bila shaka atachukuliwa hatua ya kisheria kwa kukamatwa na kufunguliwa mashtaka.
Kupitia taarifa kwa vyombo vya habari, gavana Ntutu alitoa wito kwa wakaazi kuunga mkono kazi za watoa huduma wote wa afya na kujiepusha na kuwashambulia haswa wakati wa mambo ya dharura hospitalini.
Matamshi yake ni baada ya wahudumu wa afya katika kituo cha Transmara Magharibi kushambuliwa na wale waliokuwa wameleta mwendeshaji mmoja wa bodaboda aliyekuwa amepata ajali.
Wakaazi hawa walipandwa na mori na kuwafumania wahudumu wa afya baada ya kuwaelezea kuwa wamkimbize mwathiriwa katika hospitali ya hadhi ya juu kwani hawakuwa na uwezo wa kumshughulikia kikamilifu.
Hatua hii ilizua vurugu kiasi cha kupelekea kituo hiki cha afya kufungwa kwa muda usiojulikana huku mwendeshaji bodaboda aliyeumia akikimbizwa hadi kituo cha afya cha kimishenari cha St. Joseph alipopatikana kuwa alikuwa ameshapoteza maisha yake alipofika.
Ntutu alitoa risala zake za rambirambi kwa jamaa na marafiki wa mwendazake huku akitilia mkazo wa umuhimu wa kufuata maagizo ya wahudumu wa afya wakati wote.
Aliendelea kusema kuwa serikali yake ya kaunti inafanya kazi pamoja na ile ya serikali kuu kwa ukaribu ili kuona kwamba wakaazi wa gatuzi la Narok wanapata huduma za afya bora kwa wakati wote.
Kupitia tukio hili, wahusika wakuu wa usalama ikiwemo kamati ya usalama ya kaunti, naibu kaunti kamishna wa eneo hili na wasimamizi wa hospitali ya Transmara walikuwa na mkutano na kuamua kuwa hospitali hii ilindwe na maafisa wa usalama usiku na mchana ili kuona kuwa huduma za afya katika kituo hiki zimerejelea kama kawaida bila kupoteza muda.
Na Emily Kadzo